ad

ad

Meya ampoza DC Bukoba

MKUU wa Wilaya ya Bukoba mkoani Kagera, Zipora Pangani, juzi alijikuta katika wakati mgumu baada ya wafanyabiashara wa mjini humo kumuumbua mbele ya tume iliyoundwa kuchunguza tuhuma za Meya wa Manispaa huyo, Anatory Amani.
Wazo la kuundwa tume ya kumchunguza meya lilitolewa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa baada ya kutokea msuguano mkali kati yakr na madiwani wa chama hicho.

Tayari tume hiyo inaendelea na uchunguzi wake mjini humo ambapo juzi ilikutana na wafanyabishara wa soko kuu ambalo ni moja ya mradi unaolalamikiwa kuingiwa mkataba na meya bila kuwashirikisha madiwani.
Tume hiyo inaundwa na wajumbe wanne; Abbas Kandoro (Mkuu wa Mkoa wa Mbeya), Dk. Rehema Nchimbi (Dodoma), Naibu Katibu Mkuu wa Tamisemi na Naibu Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Taarifa kutoka mjini Bukoba zilisema kuwa kikao hicho kati ya tume na wafanyabiashara kilipamba moto huku wakishinikiza kuwa meya Amani lazima ang’oke kutokana na kutumia mabavu na hivyo kuisababishia halmashauri hasara.
Wakizungumza kwa simu na gazeti hili jana, baadhi ya washiriki wa kikao hicho walisema kuwa hata mkuu wa wilaya, Pangani alilazimika kuwaomba radhi wafanyabishara hao kwa kile alichodai kuwa alidanganywa na meya kuhusu mradi huo.

“Huyu mkuu wa wilaya alidanganywa maana baada ya sisi kukataa ubabe wa meya kutaka kutuondoa kwa nguvu sokoni hapo, alikaribishwa katika mkutano kwenye Uwanja wa Kataba ambao meya alidai kuwa umeweka uongozi mpya wa soko,” alisema mtoa taarifa wetu.
Kwamba baada ya Pangani kuelezwa ukweli huo mbele ya tume kuwa alidanganywa, alilazimika kusimama na kuwaomba radhi wafanyabiashara hao.
Katika kikao hicho kilichochukua takribani saa tano, inaelezwa kuwa wafanyabishara walisema kuwa hawapingi mradi huo wa ujenzi wa soko la kisasa bali wanakataa ubabe wa meya Amani.

“Tumeieleza tume kuwa tuko tayari kufuta kesi tuliyoifungua dhidi ya meya ikiwa atang’olewa na kuchaguliwa mwingine. Maana tangu kuanza kwa vitisho vyake vya kutaka kutuondoa, biashara imeyumba. Tulichukua mikopo lakini tumepata hasara.
“Baada ya kufungua kesi, halmashauri imekuwa haikusanyi chochote kutoka kwetu na hivyo imepoteza mapato ya zaidi ya sh milioni 100. Meya alikurupuka kutufukuza wakati hakukuwa na maandalizi yoyote ya ujenzi kwani fedha za kutekeleza mradi huo hakuwa nazo,” alisema mfanyabiashara mmoja.
Jana asubuhi tume hiyo ilikutana na Baraza la Madiwani na mchana ilifanya kikao na wadau wengine wa sekta ya ardhi kusikiliza maoni yao kuhusu utekelezaji wa mradi wa upimaji na uuzaji viwanja zaidi ya 5,000.
Hata hivyo, habari kutoka Bukoba zilidai kuwa tume hiyo imekuwa ikifanya kazi yake kwa usiri mkubwa na hivyo kutotoa nafasi kwa wananchi wengi kutoa maoni yao kuhusu sakata la tuhuma hizo.

Chimbuko la mgogoro lilitokana na madiwani wanane wa CCM akiwemo na mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki na wawili wa CUF kusaini hati ya dharura kumtaka mkurugenzi wa halmashauri kuitisha kikao cha kumng’oa meya Amani.
Hatua hiyo ilisababisha uongozi wa CCM Taifa kuingilia kati na kuwaamuru madiwani wake waondoe tuhuma zao na hivyo kuiomba Tamisemi iunde tume kuchunguza miradi hiyo mitatu ya uuzwaji wa viwanja, ujenzi wa soko na stendi ya kisasi.
Mwishoni mwa wiki, tume hiyo ilikutana na madiwani wa CCM na wajumbe wa kamati ya siasa ya wilaya, jambo lililodaiwa na baadhi ya madiwani kuwa ni mkakati wa kutaka kuwalainisha ili kumbeba meya Amani.
Chanzo chetu kilidokeza kuwa wiki moja kabla ya tume kuanza kazi yake, meya Amani kwa kushirikiana na mkurugenzi aliyehamishwa, Hamis Kaputa, walimuita kazini katibu wa vikao vya madiwani mstaafu, Tukelia Kagumisa kwa muda wa wiki moja.
“Huyu mama alistaafu Januari mwaka huu, sasa kitendo cha kumwita na kujifungia naye ofisini kwa wiki nzima kinatia shaka kuwa huenda walikuwa wakibadilisha mihutasari ya vikao vilivyopita ili kupoteza ushahidi,” alisema mtoa taarifa.
Powered by Blogger.