ad

ad

MAZOEZI YA VIUNGO: Dawa bora kwa wagonjwa

MIONGONI mwa huduma ambazo bado hazijafahamika kwa wengi ni matibabu ya mazoezi ya viungo vya mwili pamoja na kuchua ‘massage’ kwa kutumia mikono na mashine za kisasa.
Salvatha Mushi, ni mtaalamu wa matibabu hayo, mwenye kituo chake maeneo ya Upanga jirani ya Ukumbi wa Diamond Jubilee, kona ya Barabara ya Nyangoro na Maliki kijulikanacho kwa jina la Pain Management Centre.
Mtaalamu huyu anasema matibabu hayo yamewasaidia wagonjwa wengi waliokuwa wamekata tamaa ya kuishi, huku akifafanua kuwa upungufu wa elimu kwa wagonjwa bado ni kikwazo.
 
Kuhusu elimu kwa wagonjwa, Mushi anasema bado ni tatizo, kwani ni wachache wanaoamini kuwa mgonjwa anaweza kupona bila kupewa dawa ya kumeza au kunywa, bali kwa kufanya mazoezi ya viungo pekee pamoja na kuchua.
“Inatakiwa kwanza mgonjwa kumpa elimu atambue kuwa mazoezi pia ni dawa. Mgonjwa anatakiwa kufanya mazoezi kadiri unavyomwelekeza, hata kama atafanyia nyumbani asipuuze maelekezo,” anasema.
Aidha, anashauri kuwa mgonjwa anapoamua kufanya mazoezi akipata nafuu asiache hadi atakapopona kabisa.

Anabainisha kwamba mgonjwa anatakiwa kufanya mazoezi kati ya siku 10 hadi 14 mfululizo na asipofikisha muda huo hata kama atapata nafuu lakini hawezi kupona.
Kuhusu gharama za matibabu, anasema kituo chake ni miongoni mwa vituo vinavyolipisha fedha chache sana, lakini wagonjwa wamekuwa wakipatiwa matibabu ya uhakika.
Anasema dawa zinazotumika katika kituo chake ni za kuchua, mashine mbalimbali za kutibu viungo na misuli, dawa za kupunguza maumivu, dawa za kushtua mishipa ya fahamu, mashine za kusaidia mzunguko wa damu na ‘massage’ ya mikono ambayo anasema ni njia nzuri zaidi.

Aidha, mtaalamu huyo anasema kuwa wana mashine za kuvuta uti wa mgongo kwa ambao ‘disc’ zimeachia, kumeguka au hazijakaa sawa. Vilevile wanatoa tiba kwa waliovunjika miguu baada ya kufanyiwa upasuaji, wagonjwa wanaowekewa vyuma na wale wanaoumwa migongo na ‘disc’ zinagusana.
Mushi anasema wanatoa matibabu pia kwa wagonjwa ambao wamepooza upande mmoja wa mwili, uso kupooza upande mmoja, ganzi kwenye mikono na miguu, kichwa kuuma, mgongo, uchovu, watoto wenye mtindio wa ubongo na watu wazima baada ya kufanyiwa operesheni ya kichwa.

Aidha, Mushi analalamikia ukubwa wa kodi inayotozwa na serikali katika kuendesha vituo vya aina hiyo na ukubwa wa gharama za vifaatiba kuwa chanzo cha malipo kuwa makubwa kwa wagonjwa na kusababisha wengi kutomudu.
“Naomba gharama za vifaa tiba na zile zinazotozwa kwa ajili ya kuendesha vituo hivi zipunguzwe ili kuwasaidia wagonjwa wengi wenye hali ya chini kumudu gharama za matibabu.

“Vilevile natoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwapo kwa vitengo vya matibabu ya mazoezi katika zahanati na hospitali za umma ili kuwasaidia wagonjwa wasioweza kugharamia matibabu hayo katika vituo vya watu binafsi,” anasema na kuongeza kuwa jambo la kusikitisha ni kwamba hata pale ambapo vitengo hivyo vipo hakuna vifaa vya kuhudumia wagonjwa.

Mushi anaitaka serikali isaidie katika kuhamasisha na kutoa elimu kwa watu mbalimbali kutambua kwamba kuna huduma ya aina hiyo ya mgonjwa kupona bila kupewa dawa isipokuwa kwa kufanya mazoezi ya viungo, hasa vijijini ambako uelewa bado ni mdogo.
Anasema kituo chake kina ubora wa hali ya juu kutokana na mwitikio wa wagonjwa wengi wanaofika hapo kupata huduma.
Mtaalamu huyo wa tiba anawataka wote wenye matatizo aliyoyabainisha hapo juu wafike katika kituo chake bila kusita kwani gharama za matibabu ni nafuu na hupungua kulingana na mgonjwa anavyojieleza.
Alikotoka Mushi

Akielezea historia fupi ya maisha yake hadi kufikia kuwa ‘Physiotherapist’ anasema alizaliwa mwaka 1972 Moshi, Kilimanjaro.
Alianza masomo ya shule ya msingi mwaka 1981 katika Shule ya Msingi Otaruni. Mwaka 1988 alianza masomo ya kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Weruweru ambako alisoma na kuhitimu kidato cha sita mwaka 1993.
Septemba 1993 hadi Mei 1996, alikuwa akisomea stashahada katika Chuo cha Physiotherapy KCMC mjini Moshi. Baada ya kuhitimu masomo alianza kazi katika Hospitali ya TMJ Mikocheni, mjini Dar es Salaam ambako alifanya kazi kwa miaka kumi, tangu Julai 1996 hadi Januari 2006.

Anasema alipoajiriwa katika Hospitali hiyo ya TMJ ndiye alikuwa mwanzilishi wa idara ya mazoezi ya viungo na akiwa mkuu wake kwa kipindi chote cha miaka 10 aliyofanya kazi katika hospitali hiyo.
“Mwaka 2006 baada ya kutoka katika Hospitali ya TMJ nilianzisha kituo changu cha Pain Management Centre kwa ajili ya kutoa matibabu ya viungo kwa njia ya mazoezi,” anasema.
Powered by Blogger.